SERIKALI
 ya Tanzania inatarajia kutuma wataalam kwenda nchini Canada katika 
Kamisheni ya Mafuta na Gesi ya jimbo la British Columbia (BC Oil& 
Gas Commission) ili kupata uelewa zaidi katika masuala ya udhibiti wa 
mafuta na gesi nchini.
Hayo yalisemwa na Naibu
 Waziri wa Nishati na Madini anayeshughulikia Nishati, Charles Kitwanga 
wakati akizungumza na watendaji wa Kamisheni ya Mafuta na Gesi ya Jimbo 
la British Columbia katika Ofisi za kamisheni hiyo zilizo katika mji wa 
Victoria nchini Canada.
Akiongoza ujumbe wa 
Tanzania uliotembelea kamisheni hiyo ili kujifunza masuala ya udhibiti 
wa sekta ndogo ya gesi asilia na mafuta, Naibu Waziri alisema kuwa lengo
 la Serikali ya Tanzania ni kuhakikisha kuwa rasilimali zilizopo 
zinaendelezwa na faida yake kuonekana kwa wananchi hivyo wataalam 
watakwenda nchini Canada katika kamisheni hiyo ili kuongeza uelewa 
katika masuala ya udhibiti ambao kwa kiasi kikubwa unachangia katika 
kuhakikisha kuwa na maendeleo endelevu ya rasilimali zilizopo Tanzania.
“Mtazamo wa wananchi 
wengi ni kuwa makampuni ya kigeni yanakuja nchini Tanzania kuchukua 
rasilimali na kuondoka nazo bila wananchi hao kufaidika hivyo serikali 
inafanya kila jitihada ili faida za rasilimali zetu ziwafikie wananchi 
wote na moja ya vigezo vya jitihada hizo ni kuwa na mamlaka madhubuti za
 udhibiti zitakazo hakikisha makampuni ya nje na ndani ya nchi yanafanya
 kazi kwa kuzingatia kanuni na sheria zinazoongoza sekta husika,” 
alisema Kitwanga.
Naibu Waziri alieleza 
kuwa Tanzania ikiwa katika mchakato wa kutengeneza sheria na kanuni 
zitakazoongoza sekta ya gesi asilia na mafuta, inahitaji kupata maoni na
 uelewa zaidi kutoka katika nchi zilizopiga hatua katika uendelezaji wa 
rasilimali hizo ikiwemo jimbo la British Columbia ambalo limegundua gesi
 asilia kiasi cha zaidi ya futi za ujazo trilioni 2,900.
Naye Ofisa Mkuu wa 
Operesheni katika Kamisheni ya Gesi na Mafuta ya British Columbia, 
Mhandisi Ken Paulson alieleza kuwa kamisheni hiyo ambayo imeanzishwa 
zaidi ya miaka 15 iliyopita ina jukumu la kudhibiti shughuli zote za 
mafuta na gesi asilia ikihusisha, utafiti, uendelezaji na usafirishaji 
wa rasilimali hizo kwa njia ya bomba.
Mhandisi Paulson 
alieleza kuwa kamisheni hiyo pia ina jukumu la kukusanya takwimu za ki 
jiolojia zinazotumika katika shughuli za utafutaji wa gesi asilia na 
mafuta na kuzitangaza kwa njia ya tenda ili makampuni yanayohitaji 
kufanya shughuli za utafutaji mafuta na gesi katika jimbo hilo yanunue 
takwimu hizo kutoka kamisheni hiyo.
Kuhusu matumizi ya gesi
 asilia, Ofisa Mkuu wa Operesheni aliueleza ujumbe huo kutoka Tanzania 
kuwa asilimia 15 ya kiasi cha gesi kilichogunduliwa katika jimbo hilo 
kinatumika ndani ya jimbo la British Columbia kwa matumizi mbalimbali na
 kiasi kinachobaki kinasafirishwa kwenda bara la Amerika Kaskazini.
Kuhusu mfumo wa 
ugawanaji mapato (PSA) kati ya kampuni ya utafutaji na uchimbaji gesi 
asilia na mafuta, Mhandisi Paulson alieleza kuwa kampuni ikianza 
uzalishaji wa gesi au mafuta, serikali ya jimbo hilo hukusanya mrabaha 
wa asilimia 10 hadi 20 ya mapato.
Katika ziara hiyo ya 
mafunzo nchini Canada, Naibu Waziri wa Nishati na Madini ameambatana na 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Victor 
Mwambalaswa pamoja na baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo akiwemo, Murtaza 
Mangungu, Raya Ibrahim, Richard Ndasa, Deogratias Ntukamazina, Shafin 
Sumar na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na Madini.
Chanzo:Majira 
 
0 comments:
Post a Comment