Home » » MBUNGE WA CCM KIZIMBANI MTWARA, ASOTA MAHABAUSU.

MBUNGE WA CCM KIZIMBANI MTWARA, ASOTA MAHABAUSU.

Mbunge wa Mtwara Mjini (CCM), Hasnein Murji (kushoto) akiingia katika chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mtwara jana kusomewa shtaka la kufanya uchochezi. Picha na Haika Kimaro.Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Simba Chawene akizungumza jambo na Mbunge wa Mtwara mjini, Hasnain Murji aliyekaa katika vikao vya mbunge mjini mwaka huu.

MBUNGE wa Mtwara Mjini (CCM), Hasnain Murji (46) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini hapa, mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Mfawidhi, Dynes Lyimo kujibu mashitaka ya uchochezi yanayomkabili.

Mbunge huyo ambaye alikamatwa siku tatu zilizopita jana alisomewa mashitaka na mwendesha mashitaka, Mwanasheria wa Serikali, Kisheni Mtalemwa akisaid
iana na Zuberi Mkakatu, na kudai kuwa Januari 19 maeneo ya Ligula mjini hapa alichochea watu kufanya vurugu kinyume cha sheria.

Murji ambaye alirudishwa rumande baada ya kukana mashitaka na kushindwa kutimiza masharti ya dhamana, anatetewa na Wakili Chaula Msechu wa Kampuni ya uwakili ya C and M Advocates ya Dar es Salaam.

Akisoma masharti ya dhamana, Hakimu Lyimo alisema mshitakiwa alitakiwa kuwasilisha mahakamani hati ya kusafiria, mdhamini mmoja mwenye mali isiyohamishika, yenye thamani isiyopungua Sh milioni 20 na iwe imefanyiwa tathmini pia asifanye mikutano yoyote ya hadhara bila kibali cha Kamanda wa Polisi wa Mkoa.

Baada ya Hakimu kusoma masharti ya dhamana, mshitakiwa alijieleza, kwamba hati yake ya kusafiria iko Dar es Salaam hivyo kuwa vigumu kwa kuiwasilisha mahakamani hapo kwa muda huo, hali ambayo ilizua mabishano ya kisheria kati ya wakili wa Serikali na wa upande wa utetezi.

Mwanasheria wa Serikali aliiambia Mahakama, kwamba kwa kuwa kuwasilisha hati hiyo mahakamani ni moja kati ya masharti ya dhamana, na kwa kuwa mshitakiwa alikiri kushindwa kuiwasilisha jana, basi Mahakama ni vema ikazingatia masharti iliyoweka na mshitakiwa apewe muda wa kutimiza masharti hayo.

“Mahakama yako imeweka masharti ambayo yamesomwa mbele ya mshitakiwa, na kuwasilisha hati ya kusafiria ni moja ya masharti yanayotakiwa kutimizwa, hivyo naiomba iyazingatie na atakapoyatimiza basi haki yake hii ya msingi ya kupewa dhamana itolewe,” alisema Kisheni.

Baada ya hoja ya upande wa Serikali, Wakili Msechu aliiomba Mahakama impe dhamana mteja wake, ili awe nje huku taratibu za kufuata hati hiyo Dar es Salaam zikifanyika, kwa kuwa mshitakiwa ni kiongozi aliyechaguliwa na watu na alionesha ushirikiano na Polisi hata pale alipotakiwa kuripoti kituo cha Polisi.

“Naiomba Mahakama yako impe dhamana mteja wangu, kwa kuwa ni kiongozi wa kuchaguliwa na wananchi, ametimiza masharti mengine, ni mwaminifu na hata alipojulishwa juu ya mashitaka yake aliripoti mwenyewe Polisi na baada ya siku mbili au tatu tutawasilisha hati hiyo hapa mahakamani,” alisema Chaula.

Baada ya hoja hizo, Hakimu Lyimo alitoa msimamo wa kisheria juu ya suala hilo ambapo alisema kwa kuwa kuwasilisha hati hiyo mahakamani ni sehemu ya masharti ya dhamana, hivyo Mahakama iliona mshitakiwa hajatimiza masharti na hivyo kurudishwa rumande hadi kesho Mahakama itakapopitia vielelezo vyake vya dhamana.

Kesi hiyo iliendelea sambamba na zingine zinazohusu vurugu za Mei 22 na 23 ambapo watuhumiwa zaidi ya 90 walifikishwa hapo kujibu tuhuma za kuhusika na vurugu hizo.

Lakini kinyume na masharti ya dhamana ya Murji washitakiwa wengine walitakiwa kuwa na mdhamini mmoja mwenye mali zisizohamishika na kutambuliwa na watendaji wa mitaa katika maeneo wanamoishi, masharti ambayo yalitimizwa na baadhi yao na walioshindwa walirejeshwa rumande.

Viongozi wengine Wakati huohuo, viongozi wanne wa vyama vya upinzani watafikishwa mahakamani hapo kwa mara ya pili Juni 13, baada ya kufikishwa katika Mahakama hiyo Juni 4 kwa mara ya kwanza wakikabiliwa na mashitaka matatu likiwamo la kula njama, kufanya uchochezi na kuamsha hisia mbaya kwa wakazi wa Tanzania.

Viongozi hao ni Katani Ahmed Katani (33) Mwenyekiti wa Vijana CUF na Saidi Kulaga (45) Katibu wa Wilaya ya Mtwara CUF, Hassan Uledi (35) Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi wa Wilaya ya Mtwara na Hamza Licheta (51) Katibu Mwenezi wa TLP wa Mkoa wa Mtwara, wote wakazi wa Mtwara.
CHANZA HABARILEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa