Home » » Tamko Maalum Kutoka Chama Cha Wananchi(CUF)Juu ya Vurugu Zilizotokea Mtwara

Tamko Maalum Kutoka Chama Cha Wananchi(CUF)Juu ya Vurugu Zilizotokea Mtwara

 
THE CIVIC UNITED FRONT- (CUF – Chama Cha Wananchi)

GHASIA ZA MTWARA

The Civic United Front (CUF – Chama Cha Wananchi) kimesikitishwa sana na vurugu zilizotokea Mtwara tarehe 22 Mei 2013 na uvunjaji mkubwa wa haki za binadamu uliofanywa na polisi tarehe 23 Mei 2013. Chimbuko la mgogoro wa gesi wa mikoa ya Lindi na Mtwara ni kushindwa kwa serikali ya CCM kutekeleza ahadi zaka za miradi ya kutumia gesi ya Msimbati na Mnazi Bay mkoani Mtwara na hasa ujenzi wa kituo cha kufua umeme wa MW 300 na kuiunganisha Mtwara, Lindi na Ruvuma katika gridi ya taifa.

CUF inalaani vikali vitendo vya kihalifu vya kuchomea nyumba ya mwandishi wa habari wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Kassim Mikongolo, na nyumba za baadhi ya viongozi wa CCM. Vile vile tunalaani vikali vitendo vya kuhujumu miundombinu muhimu likiwemo daraja la Mikindani linalounganisha Mkoa Mtwara na Mikoa ya Lindi, Pwani na Dar es Salaam.

CUF imesikitishwa sana na taarifa za vifo vya askari wanne wa JWTZ kwa ajali ya gari iliyotokea Kilimahewa wakati askari hao wakisafirishwa toka Nachingwea kwenda Mtwara kusaidia kudhibiti vurugu.Tumepeleka salamu za pole kwa CDF Jenerali Mwamunyange na kupitia kwake kwa familia za marehemu. Tunawapa pole askari wote waliojeruhiwa na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu wapone haraka na waweze kurejea katika ulinzi wa taifa letu.

Vilevile tumesikitishwa na kifo cha raia wawili kwa kupigwa risasi akiwemo mama mjamzito na raia wengi kujeruhiwa. Tunawapa pole familia za marehemu na kuwaombea wote waloumia wapone haraka na waendelee na shughuli zao.

Taarifa za vyombo vya habari vinaeleza kuwa ghasia hizi zilianza baada ya hotuba ya bajeti ya Waziri wa Nishati na Madini iliyosomwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kusisitiza ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi toka Mtwara kwenda Dar es Salaam.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa