Home » » MAKALA MAALUM KUTOKA MTWARA: GESI YA MTWARA NA MAANDAMANO: NANI HAMWELEWI NANI? SOMA HAPA

MAKALA MAALUM KUTOKA MTWARA: GESI YA MTWARA NA MAANDAMANO: NANI HAMWELEWI NANI? SOMA HAPA




                                             
Siku ya Alhamisi, Disemba 27, 2012, mkoani Mtwara, lilijiri tukio ombalo, kwa watawala       wetu,halikufikirika, halikutegemewa    na katu halikutazamiwa. Wananchi wa eneo hilo waliingia barabarani kudai manufaa ya gesi asilia iliyoko Msimbati, Mtwara vijijini.  kwa mujibu wa wana Mtwara  gesi hiyo ilikuwa inasafirishwa Dar es Salaam bila wao kubainishiwa watakavyonufaika .

Tukio hili lilileta mshtuko wa volteji kubwa (high voltage shock) serikalini. Mkuu wa Mkoa huo Kanali Joseph Simbakalile, alikuwa wa mwanzo kutoa kauli. Waandamaji  na waratibu  (vyama vya  upizani ) walipewa lebo ya “wahaini na wapuuzi”.  Kwa mujibu wa  Kiswahili sanifu, “uhaini ni tendo la kusaliti nchi yako au / kufanya  mipango ya kupindua serikali halali iliyopo madarakani”. Na upuuzi ni jambo au tendo lisilo la maana  au la kijinga. Naye Waziri wa  Nishati na Madini  Profesa Dr. Sospeter Muhongo akajitokeza : naye akasema madai ya waandamanaji yanataka kuigawa nchi ( Tanzania ) vipande vipande.
Rasilimali ya nchi ni kwa manufaa ya nchi; hilo linaeleweka kwa kila mtu.Mifano aliyotoa ya katani (mkonge)iliyolimwa Morogoro na Tanga kuwa iliwanufaisha watu wa Mtwara ina upogo. Profesa angejua kuwa mkonge umelimwa Ubena zomozi (Pwani ) na huko kusini kulikuwa na mashanba  Mikindani, Kitunda, Mkwaya, Ngurumahamba na Kikwetu . Uwanja wa ndege wa Lindi umezungukwa na shamba hilo la  Kikwetu. Kwa nini watu wa Mtwara hawajasema  maduhuli  ya korosho yatumiwe huko kusini tu? Kauli za viongozi wa serikali hazijagusa kiini au msingi wa madai ya watu wa Mtwara. Watawala wametumia shoka mahali ambapo  ukucha ungestahiki.

“Uhaini na upuuzi” wa wana Mtwara umesimama katika miguu ya historia. Kimantiki walichosema ni kuambia serikali yao “mpaka hapa si zaidi” (this farther  and no  further). Kuwaelewa watu hao hatuna budi kutalii mazingira yaliyowasukuma kufanya walivyofanya. Wanakinyongo  kilichorundikana kwa muda mrefu. Hawakuwa  bado wamepata mahali pakuegemea  na  kuyatoa  yaliyokuwa  yanawakera na kuwasibu. Walatini wamesema  “Veritatis vos liberabit “ ( ukweli utatuweka  huru); hivyo kuibua usuli na mazingira ya ukweli kutaepusha kuwaelewa watu  hao  kwa mtazamo hasi.

Kusini na buti la Wadachi (Wajerumani)
Vita  vya MajiMaji  (1905 – 1907 ) vya kupinga  utawala wa Wajerumani vilianzia  Nandete, wilayani Kilwa, mkoani  Lindi Mashamba  ya pamba yalihujumiwa , na harakati za wazalendo  hao zilienea maeneo   yote ya kusini ya mto Rufiji na kati ya Bahari ya Hindi na Ziwa Nyasa. Kipindi  kifupi tu baada ya upinzani dhahiri  kuanza askofu Cassian  Spiss ( Mswisi – wananchi  walimweka katika  kundi la Wajerumani)  aliuawa  akiwa njiani kuelekea  Liwale . Huko Nyangao ( Lindi) misheni  ya Wajerumani  ilishambuliwa na wapiganaji. Masista  wawili wa Kijerumani waliuawa baada ya kudhalilishwa na kuteswa na Waafrika.

Mwaka  1902 huko Kitangali  (Newala) Mkulungwa (kiongozi ) Mkoto aliwahamasisha wananchi wasilipe kodi kwa Wadachi. Wale ambao wangelipa wangepata maradhi ya ndui. Ujumbe ulieleweka na wananchi  wakaacha kulipa kodi. Wajerumani  wakatuma kikosi maalumu cha  askari kutoka  Lindi kumshughulikia kiongozi huyo. Alikamatwa na kunyongwa hadharani .

Kama tulivyosema upinzani  wa Wadachi ulikuwa  umeenea sana kusini.  Kwenye uwanda wa  Makonde wananchi waliwaunga  mkono wazalendo wenzao. Mwaka  1907 kikosi cha  mamluki kilitumwa toka Lindi ( makao makuu ya watawala katika sehemu hizo ) kwenda kuuzima uasi
Walipokuwa wanaelekea kwenye lengo wananchi wakapata habari za ujio huo. Walipokuwa katika kijiji cha Mtopwa (Newala) walivamiwa na wananchi. Askari wote waliuliwa wakazikwa pamoja .Mahali hapo pako katikati ya kijiji cha Mtopwa. Tukio hilo lilikoleza hasira, ghadhabu na ukatili wa Wajerumani.
Askari wengine walipelekwa kumsaka kiongozi wa  Mtopwa aliyeitwa Mtumba bin Omari. Alikamatwa na kupelekwa Lindi ambako aliteswa na hatimaye kunyongwa. Kaburi lake liko Lindi mjini sehemu iitwayo Mikumbi.

Hii ni sehemu ya katalogi ya matukio ambayo yalichefua utawala wa Wajerumani kwa eneo la kusini. Hivyo wakati sehemu nyingine za nchi zikisonga mbele kidogo huko kusini waliwekwa kwenye kifukofuko (cocoon0.

Kusini chini ya Waingereza
Baada ya Wajerumani kuangushwa duniani pote katika Vita Vikuu vya  Kwanza  vya Dunia (1914 – 1918), Tanganyika, iliyokuwa sehemu ya Dutch East Africa (nchi nyingine katika eneo hili zikiwa Rwanda na Burundi) iliwekwa chini ya utawala wa Waingereza kama wadhamini. Nchi haikuwa koloni kama ilivyokuwa Kenya, Nyasaland( Malawi) na Northern Rhodesia (Zambia). Kwa maeneo ya kusini hali ilikuwa kama Wadachi waliwaambia cha kuwafanyia wenyeji wa kusini. Hakuna kumbukumbu zinazoonyesha kwamba watawala wapya walikuwa na mipango au azma ya kuendeleza eneo hilo  katika fani mbali mbali. Yaliyotokea yalilenga kunufaisha watawala.

Baada ya vita Waingereza walikuwa wachovu kiuchumi hali ya huduma za kijamii ziliathirika na vita. Kampuni iliyoitwa Overseas Food Corporation ilianzisha mradi mkubwa wa kulima karanga Urambo (Tabora) Kongwa (Dodoma) na Nachingwea (Lindi). Ili kuhudumia mashamba kwa ufanisi bandari ya Mtwara iliboreshwa. Wakati huo huo wakajenga reli na bomba la mafuta toka bandarini Mtwara hadi Nachingwea. Reli ilikuwa ienddelee hadi Mbamba bay pwani ya ziwa Nyasa.
Mnamo mwezi Oktoba 1961 lilifunguliwa tawi la reli la kilomita takribani 40, toka Chilungula hadi Masasi. Miundombinu na shughuli za kilimo zilitoa ajira na maeneo yaliyopitiwa na miundo msingi hiyo yalifunguka kwa maendeleo
Kwa sababu mbali mbali mradi wa karanga Nachingwea ulifungwa. Mwaka mmoja baada ya Tanganyika kupata Uhuru, sarikali ya Tanganyika huru ikaamini kuwa reli na bomba la mafuta vilikuwa ni miradi isiyo na tija. (white elephant). Reli na bomba vikang’olewa. Athari za hatua hiyo ni bayana .Kusini kulizidi kuzama kimaendeleo, taswira iliyodumu kwa kipindi kirefu. Lakini kwa muda mfupi watawala  (Waingereza) walimaizi kwamba eneo la kusini lilikuwa na utajiri mwingi hivyo wakaita “Cinderella  Province” Cinderella ikiwa na maana ya ‘mtu au kitu ambacho uzuri au uwezo wake haujatambulikana”.

Jingine  walilolifanya Waingereza  ni kuangusha magogo na kupasua  mbao huko Rondo Mnara (Lindi  vijijini). Kampuni  iliyoitwa Steel Brothers  ilifanya kazi hiyo miaka ya 1950. Wakavuna , wakachuma na  kuondoka . Wananchi wakaachiwa visiki vya  mipingo , mbambakofi,mivule  nk. wakati huo huo  walikumbatia umasikini.
Kusini baada ya uhuru.
Miaka  michache ya kuelekea uhuru kulianzishwa mradi mkubwa wa maji toka  mto Ruvuma ,uliendeshwa na kampuni ya Makonde Water  Corporation. Ilipangwa maji yaenezwe sehemu mbalimbali  huko kusini. Miaka michache baada ya kuasisiwa kwa vishindo  mradi ulikufa. Wananchi  hawakuelezwa sababu  za mabadiliko hayo.  Madhila , taabu na kero za kukosa maji hazikumilithika .

Katihati ya miaka 1960 kulizuka mgogoro wa kiwanja katika mji mdogo wa Mahuta  (wakati huo Newala , sazsa uko katika wilaya ya Tandahimba ). Mfanyabiashara wa  Kiasia alipora eneo hilo ili ajenge kituo cha mafuta ya nishati. Wananchi wakachachamaa. Uongozi wa mkoa na wilaya ukaingilia kati. Kwenye  mkutano wa hadhara hapo Mahuta , kiongozi wa wananchi alipigwa viboko kwa sababu za “kupinga hatua za maendeleo “ kama walivyoita watawala. Kupinga uonevu  kunyanyaswa na kudharauliwa,  wananchi waliandika  barua ngazi za juu za taifa na kudai , moja , mkuu wa mkoa na yule wa wilaya wahamishwe ,mbili, wapendekeze majina ambayo yatatoa mkuu wa mkoa  na yule wa wilaya ; na tatu kama maombi hayo hayatakubalika watajitenga na kujiunga na Msumbiji ili wawe pamoja na FRELIMO kutafuta ukombozi. Yaliyofuata ni historia.
Miaka  mitatu baada ya uhuru wa Tanganyika , wana Msumbiji kupitia  FRELIMO walianzisha vita vya ukombozi. Kutokana na  mazingira ya kijiografia ( kati ya nchi mbili ) eneo lote la kusini likawa “no go area” – hapakuwa na shughuli zozote za maana za kimaendeleo  zilizokuwa  zikifanyika . FRELIMO  wakafanikiwa kukunja jamvi ukoloni mwaka 1975. Ni dhahiri kwa miaka kumi wengine walikuwa wamesonga mbele hapa nchini . Mategemeo na matumaini ya wengi huko kusini ni kuwa serikali ingekuwa na  programu  maalum “kufidia muda uliopotea”. Wakati wa Vita kuu ya Pili vya dunia Yugoslavia ilipambana na majeshi    ya Adolf  Hitler . Marshal  Josef Tito akawaambia wapiganaji wale  “ The wounded should not be  left behind “  ( majeruhi wasiachwe nyuma). Kimaendeleo  kusini ilijeruhiwa na kuachwa nyuma.

Barabara  ya Dar es salaam – Lindi ni “mkunga” wa matatizo ya kusini. Ahadi  za serikali kuijenga  zimechukua  kipindi kirefu kutekelezwa. Miaka  ya 1970 – 80 kampuni moja ya Kitanzania  na taasisi moja ya serikali waliteuliwa kujenga barabara hiyo. Wakajenga  makambi  Nangurukuru (Kilwa).Hakuna ushahidi wa kazi   iliyofanywa – tatizo la barabara likawa “ kichwa cha mwenda wazimu”. Mwaka  1977 wananchi wa  kusini, wakiungwa mkono na  wa maeneo mengine, waliasisi  mchango  maalum kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo. Mwitikio wa wito huo ulikuwa chanya. Ofisini ya  Waziri  Mkuu ikasitisha zoezi hilo kwa ahadi kuwa  serikali igejenga   mradi huo. Imechukua  miongo kadhaa kukamilika kazi hiyo.

Miaka ya 1960 – 70 wananchi  wa kusini  walihamasishwa kulima korosho kwa ajili ya biashara. Matokeo yalikuwa ya kutia moyo. Mapori  yalipisha mashamba ya mikorosho. Zao likachangia umasikini. - Pembejeo bei juu na soko likawa  halina  uhakika .
Kuna viwanda vya  kubangua  korosho  Masasi , Newala  Lindi na  Mtwara lakini hakuna  msimamo  maalum wa Bodi ya Korosho na wanasiasa wa kuuza nje zao lililoongezewa thamani. Bado wanakumbatia fikra hafidhina zilizopitwa na wakati wa kuuza nje ya nchi korosho ambazo hazijabanguliwa.

Alama za nyakati na Baba Kundambanda.
Walioandamana huko Mtwara walikuwa wanadai haki waliyoikosa kwa  miaka mingi. Kilichoonekana  kama  uhaini na upuuzi  ni mbegu ya tunda ya mti wa ahadi  zisizotekelezwa. Kwa  wachunguzi wa mambo dalili zilianza kujitokeza  mapema mwaka 2012. Msanii  mmoja wa huko kusini alitoa nyimbo zinazochambua uadilifu wa polisi, EPA, sera nzuri za  Mwalimu Nyerere na wanasiasa   wa maeneo  ya kusini wanavyo waona wananchi kuwa ni mazuzu . Nyimba  za   msanii huyo, Baba kundambanda, anaimba kwa lafudhi ya Kimakonde,  moja ya lugha za kusini na pia huingiza maneno  ya lugha hiyo kwa mfano  anasema viongozi / wanasiasa huwaambia wananchi kuwa koromeo   lilkipanda na kushuka maelezo yake ni  kuwa  shetani anatwanga mtama  ( Nandenga atwangi ntama pang’ulo ) . lakini wananchi kwa kuwa si “ mavelu “ (mazuzu, wajinga ) hujibu  “ kulambila” ( huo ni uongo ). Wimbo huu una  umarufu mkubwa na jijini  Dar es salaam huchezwa na baadhi ya vituo vya redio.

Nani  hamwelewi nani ?
Maelezo ya Waziri Muhongo kupitia vyombo vya habari hayajibu hoja ya msingi ya madai anayoyapuuza. Yakichambuliwa kwa uyakinifu na mantiki ni kama kuhamisha magoli ili mabao yasiingie kimiani. Takwimu  anazotoa zipo kando ya madai ya wananchi – tutanufaikaje? Kama ni zile ahadi za “yatakayofanywa baadaye”  ndiyo yanayewapa watu hao nguvu  ya  kutamka “ mpaka hapa si zaidi”  kwa sababu  wamepitia mengi  ya ahadi zisizotelekezwa. Msamiati  wa vitisho hautapunguza ari ya wananchi  kutoa maoni na madai.

Makala  inahitimishwa kwa aina mbili za semi  ambazo ni maarufu  sana katika eneo hilo la nchi. Watu wakipeana mikono kisha  mkono mmoja  ukaacha viganja na kuelekeza kwapani mtu huyo ana lake jambo. Anayedai kuendelezwa hawi haini au mpuuzi – mkono unaelekea kwapani. Mahusiano ya ukwe ni ya heshima kubwa sana katika jamii za Watanzania: - usemi wa pili  -kijana  wa kiume alikuwa anavuka kijito kwa miguu na mama mkwe: mama mkwe alikuda ili nguo zake zisirowe na kwa kufanya hivyo mapaja yake yakaonekana. Katika usemi huu badala ya kijana weka neno wana Mtwara na mama mkwe weka “viongozi wa serikali/ wanasiasa”. Nani kaonesha kisichostahiki?


             Ronald M Munga
                                                        
                                                                                           
        
                                
                                                       
        
   

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa