Home » » JIPANGE WALIA CCM KUWANYIMA ENEO

JIPANGE WALIA CCM KUWANYIMA ENEO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 
KIKUNDI cha Jipange cha kinamama wajasiriamali mkoani Mtwara, wameilalamikia Ofisi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa, kwa kutowapa sehemu ya kufanyia biashara zao licha ya kuwa wa kwanza kufika katika eneo hilo.
Akizungumza na Tanzania Daima jana kwa uchungu maeneo ya Bima wanapofanya baishara yao, Mwenyekiti Msaidizi wa kikundi hicho, Amina Maulidi, alisema kuwa walifika eneo hilo la biashara kipindi kirefu wakati pakiwa na pori.
“Hili eneo ni la CCM na tulipofika hapa tulilikuta chafu na hakuna hata banda moja, baada ya sisi kuingia kama miaka sita mbele, wakaja watu wa CCM kugawa viwanja kwenye eneo hili, lakini cha kushangaza sisi akinamama wametukuta na wametuona lakini wametunyima kiwanja,” alisema Amina na kuongeza.
Tulipeleka barua CCM Mkoa mwaka 2010 hatukupata majibu yoyote hadi leo, wakati eneo hili tumesafisha, sisi tulikuta pana pori kweli, hapa tulipo hatuna kiwanja wala hatuna eneo la kufanyia biashara ya kudumu…eneo hili tunalofanyia biashara ni la huyu baba mwenye hii sheli, baada ya kutuonea huruma tunahangaika ndipo alipotuambia tujenge hii sehemu lakini tusijenge banda la kudumu kwa sababu wakati wowote anaweza kutuambia anataka eneo lake.
Hata hivyo, Amina alisema kuwa kama mwenye eneo akilitaka, watakuwa hawana tena sehemu ya kufanyia biashara yao na ikishindikana kabisa, watakwenda kupanga biashara yao mbele ya ofisi ya CCM Mkoa au ofisi ya Mkuu wa Mkoa, kwa sababu biashara hiyo ndiyo inayowaendeshea maisha yao ikiwemo kulipa kodi ya nyumba pamoja na kusomesha watoto wao.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa kikundi hicho, Asha Kumpeta, alisema kuwa kikundi chao kilianza biashara mwaka 2000 katika eneo hilo la CCM na walilikuta eneo hilo likiwa chafu, wakawa wanalima wanaweka meza chini ya mwembe wanapanga bidhaa zao.
“Sisi tulishaandika barua na kupeleka CCM Mkoa, lakini baada ya miezi kama nane au tisa walikuja kugawa viwanja sisi tulikosa, tukaenda tena kwa katibu wa CCM kufuatilia na tulipowauliza kwa nini tumekosa kiwanja, walitujibu subirini kuna eneo limebaki kama maeneo tatu hivi tutawapatia,” alisema Kumpeta na kuongeza:
Lakini baada ya kuona kimya, tulienda tena wakatuambia lile eneo limeshachukuliwa, kiukweli tuliumia sana ila hatukuwa na jinsi…Ombi letu sisi Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali mstaafu Joseph Simbakalia, atakoposikia kilio chetu tunaomba atusaidie sisi akinamama eneo la kufanyia biashara na liwe la kwetu na la kudumu, kwani uwezo wa kujenga wenyewe tunao kinachotakiwa tupatiwe tu eneo.
 Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa