Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, amekutana na ufisadi katika utoaji wa zabuni wa ujenzi wa gati mpya tatu Bandari ya Mtwara.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa
vyombo vya habari jana, ufisadi huo alikutana nao Jumamosi iliyopita
wakati akiwa kwenye ziara bandarini hapo, akikagua eneo la ujenzi wa
gati hizo.
Taarifa hiyo ilisema, Majaliwa alieleza ana taarifa kuhusu
utolewaji wa zabuni hiyo na mzabuni ameshashinda lakini kuna madai
kwamba watu wa manunuzi kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma
(PPRA) ndiyo wanakwamisha zabuni hiyo.
Kutokana na hilo, Waziri Mkuu aliwataka wabunge wa mkoa wa Mtwara
washirikiane kusimamia suala hilo ili ujenzi wake uweze kuanza mara moja
na kuzalisha ajira kwa wananchi wa mkoa huo.
“"Ujenzi ukikamilika siyo tu ajira zitaongezeka, bali hata meli
nyingi zitaleta mizigo katika bandari hii na mapato ya mkoa
yataongezeka,” ilisema taarifa hiyo ikimnukuu Waziri Mkuu na kuongeza:
“Natambua kwamba kuna mpango wa kujenga gati nne, ambazo moja kati
ya hizo itajengwa na TPA (Mamlaka ya Bandari), lakini hizi tatu
zilitangazwa na kupata mzabuni ambaye ni kampuni ya Hyundai kutoka Japan
lakini imekuwa ikizungushwa bila sababu. Tutafuatilia kubaini tatizo
liko wapi.”
“Sasa hivi tuna uwezo wa kupaki meli moja tu, lakini gati hizi
zikikamilika tutaweza kuwa na meli tatu kwa mpigo, cha msingi tusimamie
maamuzi yetu kwamba lazima wafanyabiashara wa korosho watumie bandari
hii kusafirisha mizigo yao na si kuipeleka kwingine.”
‘MAJIPU’ BODI YA KOROSHO
Waziri Majaliwa alisema kwenye Bodi ya Korosho nako kuna majipu yanahitaji kutumbuliwa.
“RCC (Kamati ya Ushauri ya Mkoa) ilishakaa na kupitisha uamuzi kuwa
mizigo yote ipitie Bandari ya Mtwara, lakini kuna watu ndani ya bodi
hiyo wanatoa vibali vya kusafirisha mizigo kupitia Bandari ya Dar es
Salaam,” alisema.
Alimtaka Mkuu wa Bandari ya Mtwara, Prosper Kimaro, awe makini na
watu wa kitengo cha manunuzi katika bandari hiyo kwa sababu ni chanzo
cha upotevu wa fedha za serikali kutokana na watu wachache.
"Hapa si kuna mtu alitaka kuiba Sh. milioni 300 kwa kufoji saini za
wakubwa wake?” alihoji Waziri Mkuu swali ambalo lilijibiwa na Kimaro
kwamba ni kweli lakini uongozi uliingilia kati kabla wizi huo
haujakamilishwa.
FIDIA
Kuhusu fidia kwa wakazi wa vijiji vya Kisiwa na Mgao ambao
wamekubali kuhama ili kupisha upanuzi wa bandari hiyo, taarifa hiyo
ilisema Waziri Mkuu alisema tayari Sh. bilioni 13.8 zimekwishatengwa na
wizara na zitatolewa mwezi ujao.
Taarifa hiyo ilisema Majaliwa alimtaka mkuu wa mkoa huo akae na
Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, ili kuweka mbinu za kuthibiti
upenyo wa uingizaji wa mchele na sukari kwenye bandari bubu kwa lengo la
kukwepa kodi.
Desemba 3, mwaka jana Waziri Mkuu alifanya ziara ya kushutukiza
katika Bandari ya Dar es Salaam na kukuta makontena 2,431 yalitolewa
bila kulipiwa ushuru, pamoja na Novemba 27, mwaka jana kubaini
utoroshwaji wa makontena 349 ambayo hayakulipiwa kodi na kuisababishia
serikali hasara ya Sh. bilioni 14.
Aidha, Februari 19, mwaka huu, kiongozi huyo alifanya ziara ya
kushtukiza katika Bandari ya Tanga na kukuta matishari tatu zikiwa
chakavu, bila injini wakati serikali ilitoa fedha ya ununuzi wa
matishari ya kisasa.
CHANZO:
NIPASHE
0 comments:
Post a Comment