Na Fatma Salum- MAELEZO,
Serikali
kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) imetenga shilingi
bilioni 10 katika mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya ukarabati wa
Uwanja wa Ndege wa Mtwara.
Hayo
yamebainishwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhe.
Edwin Ngonyani leo Bungeni Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa
Mtwara Vijijini Mhe. Hawa Ghasia lililohoji kuhusu ukarabati wa Uwanja
wa Ndege wa Mtwara.
Mhe.
Ngonyani alisema kuwa Serikali imeendelea kufanya matengenezo ya mara
kwa mara katika uwanja huo na TAA inafanya tathmini ya uchakavu wa
matabaka ya lami (Pavement Evaluation) ya njia ya kuruka na kutua ndege
ili kubaini ukarabati stahiki unaotakiwa na matumizi ya fedha
zinazohitajika na kazi hiyo ya tathmini inatarajiwa kukamilika ifikapo
Juni 2016.
Aidha,
Mhe. Ngonyani alieleza kuwa katika mpango wa muda mrefu, Serikali
kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege inaandaa Mpango Kabambe (Master
Plan & Concept Design) kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa uwanja
huo kutoka daraja 3C la sasa kwenda daraja la 4E ili kuweza kuhudumia
ndege kubwa zaidi hivyo kuwa kitovu cha usafiri wa anga kwa Ukanda wa
Kusini.
“Ukarabati
na upanuzi wa uwanja utahusisha miundombinu yote ya kiwanja ikiwemo taa
na mitambo ya kuongozea ndege pamoja na majengo. Kazi hiyo ya uandaaji
wa Mpango Kabambe na Usanifu wa Awali inatarajiwa kukamilika Julai
2016.” Alisema Ngonyani.
Ikiwa
ni mpango wa muda mfupi, Mhe. Ngonyani aliongeza kuwa Mamlaka ya
Viwanja vya Ndege imeingia makubaliano na Kampuni ya British Gas (BG)
kwa ajili ya kutumia taa zake ambazo ni za kuhamisha kwa ajili ya
kuongozea ndege pale ambapo ndege itatakiwa kutua usiku katika uwanja
huo.
0 comments:
Post a Comment