Home » » TPDC YATOA MADAWATI 500

TPDC YATOA MADAWATI 500

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Dk James Mataragio
SHIRIKA la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limetoa msaada wa madawati 500 kwa kata ya Madimba wilaya ya Mtwara.
Msaada huo umefanya kata hiyo ifanikiwe kukamilisha agizo la Rais John Magufuli kwa asilimia 100, hivyo kutokuwa na wanafunzi wanaokaa chini.
Kata hiyo ya Madimba ndipo kwenye kiwanda cha kuchakata gesi, inayosafirishwa kwa bomba la gesi mpaka jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa TPDC, Dk James Mataragio alimkabidhi madawati hayo Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Halima Dendego katika shule ya msingi Madimba na kushuhudiwa na viongozi wa mkoa na wilaya.
Dk Mataragio alisema katika kuendelea kutekeleza dhana ya uwajibikaji, TPDC imechangia madawati 500 kwa halmashauri ya Mtwara Vijijini, lengo likiwa ni kumaliza tatizo la wanafunzi kukaa chini wakiwa darasani.
Alisema kwa kutumia madawati hayo, utasaidia wanafunzi kupata elimu bora na hatimaye kupata wataalamu watakaokuja kufanya kazi katika sekta ya mafuta na gesi hapo baadaye.
Akizungumzia suala la madawati wilayani hapo, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Vijijini, Fatma Ally, alisema baada ya msaada huo wa madawati, kata ya Madimba imekamilisha agizo la Rais kwa asilimia 100 huku kata ya Mkubiri ikibaki na uhaba wa madawati 14, ambayo atayanunua yeye na wao kuwa wamekamilisha uhaba huo.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Vijijini, Denis Kitali alisema wilaya hiyo ina shule 67 za msingi na sekondari huku kukiwa na upungufu wa madawati 5563 kutokana na mahitaji ya madawati 13,155 na sasa wanayo madawati 7562.
Alisema kwa kushirikiana na wadau mbalimbali na kukarabati madawati yaliyokuwa yakiharibika, watahakikisha wanakamilisha agizo la Rais kutokuwa na mwanafunzi anayekaa chini.
Dendego alisema watahakikisha wanatekeleza agizo hilo la Rais kwa asilimia 100, ingawa bado kuna changamoto.
Lakini, aliwaagiza watendaji wake kuwa kabla yeye hajatumbuliwa, basi atakuwa ameishawaondoa wao. Hivyo kwa kushirikiana, wameanzisha programu mbalimbali zitakazowezesha kupata madawati katika shule zote ikiwa ni pamoja na kuwaomba wadau mbalimbali kuwasaidia kufikia malengo.
CHANZO: HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa