Home » » CUF: CCM IMEMUONEA EDWARD LOWASSA.

CUF: CCM IMEMUONEA EDWARD LOWASSA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa

Chama  cha Wananchi (CUF), kimeibuka na kumtetea aliyekuwa Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa (pichani juu), kwamba Chama Cha Mapinduzi (CCM), kilimuonea kwa kukata jina katika ngazi ya Kamati ya Maadili na kushindwa kulifikisha  Kamati Kuu ya CCM (CC).
 
Lowassa alikatwa jina lake akiwa ni miongoni mwa wagombea 38 wa urais kupitia CCM, lakini inadaiwa kwamba aliondolewa katika hatua za awali kwenye Kamati ya Maadili.
 
Kadhalika, CUF kimesema kipo tayari kumpokea Lowassa ndani ya chama hicho kwa kuwa ni msafi na hajawahi kufikishwa hata mahakamani kwa ajili ya kushitakiwa kutokana na madai ya rushwa.
 
Kauli hiyo ilitolewa jana na Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CUF, Abdul Kambaya, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Pilikapilika za uchaguzi nchini kinachorushwa na kituo cha Televisheni cha Star Tv.
 
Kambaya alirejea ripoti ya Kamati teule ya Bunge iliyoongozwa na Dk. Harrison Mwakyembe mwaka 2008 kuchunguza kashfa ya Richmond ambayo ilimng'oa Lowassa katika nafasi ya Waziri Mkuu.
 
Alisema katika kamati hiyo, Dk. Mwakyembe aliweka bayana kwamba kila mtu aliyehusishwa ama kutajwa katika kashfa ya Richmond angefikishwa mahakamani kujibu mashtaka.
 
Kambaya alisema mpaka sasa Lowassa hajawahi kufikishwa mahali popote kushitakiwa na kwamba hatua hiyo inaoonyesha kwamba kiongozi huyo hakuwa na kashfa yoyote.
 
Alisema lengo la CUF ni kuing'oa CCM na kwamba ukiona kuna mtu mwenye uwezo mkubwa wa kuitikisa chama hicho na kukipasua wapo tayari kumkaribisha ili washirikiane naye.
 
Alifafanua kuwa mtu ambaye siyo msafi hawezi kukaribishwa CUF na kwamba Lowassa kama angekuwa mchafu angekuwa ameshitakiwa mahakamani tangu alipojiuzuru mwaka 2008. Katika mjadala huo washirki walijadili matumizi makubwa ya fedha yaliyojionyesha ndani ya CCM tangu mchakato wa kuelekea Uchaguzi Mkuu ulipoanza. 
 
Watu wengine waliojitokeza kumtetea Lowassa ni pamoja mwanachama mwenye kadi namba nane ya CCM, Kingunge Ngombale Mwiru, ambaye alitamka wazi kwamba kanuni na sheria ndani ya chama zilikiukwa.
 
Kingunge alisema haki haikutendeka kwa sababu Kamati ya Maadili kwa mujibu wa kanuni na taratibu za CCM haina mamlaka ya kukata jina la mgombea kwa sababu siyo kikao cha maamuzi. Wakati hayo yakisemwa, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye amewaonya watu wanaokisema vibaya chama hicho na kwamba kitawachukulia hatua.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa