Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mhe; Stephen Wasira akisaini kitabu cha wageni ofisi za CCM Mkoa wa Mtwara
WAZIRI
wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira,amewahimiza wakazi wa
Mtwara kuwekeza katika uzalishaji wa mazao ya kilimo na uvuvi ikiwa ni
sehemu ya shughuli za kiuchumi zitakazowanufaisha kutokana na
kugundulika kwa gesi asilia katika ukanda wa kusini mwa nchi.
Wasira
ambaye pia ni Mbunge wa Bunda alikuwa akizungumza na wanachama wa Chama
Cha Mapinduzi (CCM) waliomdhamini ili apitishwe na chama hicho kuwania
Urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Alisema
ingawa zipo fursa nyingi zitakazowanufaika Watanzania kutokana na
sekta hiyo mpya (gesi), lakini mazao ya kilimo na uvuvi yanaweza kuwa
miongoni mwa shughuli zitakazowanufaisha wananchi wengi hasa wa hali ya
chini.
Mtwara
ni eneo lililowahi kukumbwa na machafuko kutokana na hisia tofauti
zilizokuwapo kuhusu manufaa yanayopaswa kuwafikia wakazi wa mkoani
Mtwara, hasa kuhusu ujenzi wa viwanda na kuibadili gesi ili
itakaposafirishwa isiwe katika mali ghafi.
Hata
hivyo, Wasira alisema anatarajia kufungua fursa nyingi zaidi za
kiuchumi kwa ajili ya wananchi kama atateuliwa na CCM na hatimaye
kushinda katika Uchaguzi huo.
Hakuelezea kwa undani kutokana na kuwa wakati wa kampeni bado haujafika, bali sasa hivi anatafuta udhamini ndani ya CCM.
Wakati
huo, Wasira na mtia mwingine, Makongoro Nyerere, wameelezea kuridhika
na namna wanavyoshiriki mchakato wa kusaka Urais kwa kutumia magari,
tofauti na watia nia waliowekeza fedha nyingi kiasi cha kutumia usafiri
wa angani katika maeneo mengi.
Waliyasema
hayo walipokutana kwenye ofisi za CCM mkoa wa Mtwara, ambapo Makongoro,
alirukaruka na kumkumbatia Wasira. Tukio hilo lilitafsiriwa kuwa ni
ishara za umuhimu wa kufanya ushawishi kwa amani pasipo kuiathiri CCM,
wanachama ama Watanzania kwa ujuma.
“Hizi
ndizo siasa tunazozitaka ndani ya CCM na Tanzania yetu, sio wagombea
wengine wanaotumia utajiri na fedha zao kuwakandamiza wadogo na kuibua
mafarakano kwenye jamii,” akasikika kiongozi mmoja wa CCM (jina tunalo)
akisema.
Wasira,
alikwenda pia katika mkoa wa Lindi ambapo alifadhiliwa. Leo (alhamis)
ataelekea mkoani Mwanza kuendelea na ziara ya kuomba udhamini kwa
wana-CCM wa mikoa ya kanda ya Ziwa Victoria.
0 comments:
Post a Comment