Home » » CUF WABAINI KASORO LUKUKI UANDIKISHAJI WA BVR KUSINI.

CUF WABAINI KASORO LUKUKI UANDIKISHAJI WA BVR KUSINI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba.
Chama cha Wananchi (CUF) kimebaini kuwapo dosari lukuki katika uandikishaji wapigakura katika Daftari la Kudumu la Wapigakura unaondelea katika mikoa ya kusini ya Lindi, Mtwara na Ruvuma.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba, alisema viongozi wa CUF walifanya ziara katika mikoa hiyo na kukuta changamoto mbalimbali zikiwamo waandishi kutokuwa na uzoefu na mashine za BVR kutofanya kazi, hali iliyosababisha wananchi wengi kukosa haki zao za msingi.
 
“Katika vituo vingi, uandikishaji ulisuasua kwa sababu waandishi wengi walionekana kukosa uzoefu, mashine kushindwa kufanya kazi inavyotakiwa,” alisema na kuongeza: 
“Hali hii ilisababisha wananchi kuachwa bila kuandikishwa. katika daftari la wapigakura.”
 
Prof. Lipumba alisema walibaini kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi(Nec) haikufanya jitihada za kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki kujiandikisha huku akisisitiza taarifa zilichelewa kufikishwa kwa wakati.
 
Aidha, alisema muda wa siku saba uliotengwa na Nec haukutosha kuandikisha wananchi wote wenye haki ya kuwa wapigakura akiiomba Nec iongeze angalau wiki mbili.
 
Alisema bajeti iliyotengwa kwa ajili ya kuandikisha wapigakura haitoshelezi kuweka waandishi wengi katika vituo kwa kuwa kwenye vituo hivyo kuna waandishi wawili wanaofanya kazi kuanzia saa 2:00 asubuhi mpaka saa12:00 jioni hali inayosababisha kushindwa kuwahudumia wananchi ipasavyo.
 
Prof. Lipumba alisema katika baadhi ya wilaya kama Tunduru BVR kits hazitumiwi kutokana na Nec kutokuwa na fedha za kutosha za kuwalipa waandikishaji huku akitaja waandishi hulipwa Sh. 100,000 kwa wiki wengi wao wakiwa wanakaa katika maeneo ambayo siyo nyumbani.
 
Aliongeza kuwa baadhi ya  vituo kulikuwa na matatizo ya kutotambuliwa kituo ambacho mpiga kura amejiandikisha na kitambulisho alichopewa akitolea mfano wilaya ya Newala kituo cha kuandikisha cha Mahoha, kadi ya mpigakura ilisomeka Nambari A  wakati kijiji cha Nambali kiko kilometa 15 kutoka kituoni hapo.
 
Alisema katika Kata ya Michemo kituo cha kuandikisha cha Mchemo A kadi ya mpiga kura ilisomeka kata ya Mpwapwa huku waandikishaji waliondolewa wakiwa wameandikisha watu 31 wakati makadirio ya kata nzima ni wapiga kura 3059.
 
Alifafanua katika Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Naibu Katibu Mkuu wa CUF Bara, Magdalena Sakaya, alishuhudia wananchi wengi ambao hawakuandikishwa katika vituo wiki ya kwanza, lakini mashine za BVR zilondolewa na kwamba alipomuuliza mkurugenzi wa wilaya hiyo hakuwa na majibu kwa wananchi.
 
Pia, katika kijiji cha Mlonde kata ya Mtemanga wilaya ya Tunduru, alisema asilimia 60 ya wananchi wenye haki ya kuwa wapigakura hawakuandikishwa na cha kushangaza mashine zilihamishwa.
 
Alisema idadi ya wapiga kura ni 2,260, lakini walioandikishwa ni 920 tu huku katika Kata ya Namwinyu kiyuo cha Uliya na Ndenyenge siku mbili za mwanzo walaindikishwa watu wanne tu.
 
Prof. Lipumba alisema ugawaji wa BVR kit hauna uwiano na idadi ya wapiga kura waliopo kwenye vituo  akitolea mfano Kata ya Majimaji wilayani Tunduru, kituo cha shule ya msingi na Chalinze kina wapigakura 8,000, lakini kila kituo kilipewa mashine moja.
 
Alisema kuna vituo vyenye wapigakura 200 mpaka 1,000 vimepewa BVR kit mbili hadi nne wakati vituo vyenye watu 2,000-2,800 vilipewa BVR kits moja.
 
Hata hivyo, Prof. Lipumba alisema  kuna mikakati ya kuonekana tume imefikia mikoa yote bila kuwapa fursa wananchi wote wenye haki ya kuwa wapigakura kujiandikisha akibainisha kuna hatari wengi wakanyimwa fursa ya kuwa wapigakura.
 
Aliitaka serikali iipe Nec fedha za kutosha kukamilisha  mchakato wa kuandikisha na kuacha kupoteza fedha nyingi katika maandalizi ya kura ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa.
 
Alipoulizwa Mwenyekiti wa Nec, Jaji Mstaafu Damian Lubuva, alisema mchakato wa uandikishaji unaendelea vizuri na dosari hizo zitatatuliwa daftari litakapokamilika kwa kuangalia maeneo husika.
 
“Niko mkoani Mtwara wilayani Masasi, uandikishaji unaendelea vizuri hakuna dosari kubwa ni ndogo ndogo ambazo haziwezi kuathiri, zitarekebishwa mara tu daftari likapokamilika, alisema Jaji Lubuva.
 
Alisema katika maeneo ambayo mashine za BVR zilionekana kutokutosheleza idadi ya wapiga kura zilichukuliwa sehemu nyingine na kupelekwa katika maeneo hayo.

CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa