Home » » Zitto: Nitamuunga mkono Mbowe

Zitto: Nitamuunga mkono Mbowe


HAKI SAWA: Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba (kulia) na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, Zitto Kabwe wakiwasili kwenye Uwanja wa Mashujaa mjini Mtwara jana, ambako walihutubia mkutano wa hadhara. Picha na Ibrahimu Yamola

Mtwara. Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe amesema atamuunga mkono Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe pale atakapowasilisha hoja yake bungeni kuhusu ufisadi wa zaidi ya Sh1 trilioni katika mradi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam.
Zitto aliyasema hayo jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Mashujaa mkoani hapa uliandaliwa na Chama cha Wananchi (CUF) kuwashukuru wakazi wa mkoa huo kwa kuwachagua viongozi wa chama hicho katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
“Najua bado mnalia kuhusu bomba la kupeleka gesi Dar es Salaam, machozi yenu yatafutika kwani tayari habari za ufisadi mkubwa katika ujenzi wa bomba hili zimeanza kuchomoza.
“Kiongozi wa Upinzani Bungeni (Mbowe) ametamka mara kadhaa kuwa atatoa hoja kuhusu ufisadi katika ujenzi wa bomba la gesi. Pale atakapohitaji msaada wetu tutamsaidia, tunaamini gharama za mradi huu zimezidishwa mara mbili na inawezekana kabisa kuwa zaidi ya Dola ya Marekani 600 milioni (zaidi ya Sh1 trilioni) zimegawanywa kwa watu kama rushwa kuanzia China mpaka hapa Tanzania. Machozi yenu wana Mtwara yatafutwa kwa uwezo wa Mola,” alisema Zitto.
Alisema katika miaka ya hivi karibuni Mkoa wa Mtwara umechukua sura mpya kitaifa baada ya kugunduliwa kwa gesi na wao (wananchi) wameonyesha kwamba wakiamua wanaweza kupigania masilahi ya Taifa.
“Mmesimama kidete kuhakikisha utajiri huu hauporwi na haturudii makosa yaliyofanyika Kanda ya Ziwa pale tuliporuhusu madini kuporwa na mabeberu wa kimagharibi,” alisema.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akiwahutubia wakazi hao, aliwataka viongozi wa Serikali za Mitaa waliochaguliwa kuongoza kwa misingi ya chama ya haki sawa kwa wote.
“Profesa Muhongo (Waziri wa Nishati na Madini, Sospeter) hana uwezo wa kuendelea kuwapo madarakani na hapaswi kufumbiwa macho, wote waliohusika na sakata hili lazima wachukuliwe hatua,” alisema.
Kuhusu uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura alisema, “watakapokuja kuwaandikisha jitokezeni hiyo ndiyo njia pekee ya kutafuta ukombozi wa pili wa Taifa hili lakini msipofanya hivyo hatutawaondoa hawa CCM.”
Mapokezi yalivyokuwa
Pilika pilika za mapokezi ya viongozi hao zilianza tangu asubuhi na ilipofika saa 5.20 zaidi ya magari 40 yaliyopambwa kwa bendera za CUF, pikipiki 300 na bajaji 30 zilikusanyika katika daraja la Mikindani kuwapokea viongozi hao.
Wakiwa wamevalia sare za chama chao, wafuasi hao walikuwa wakiimba nyimbo mbalimbali ukiwamo wa “Tunataka fedha zetu za escrow zirudi... mtumbwi wa Chenge umetoboka.’
ACT wapata kipigo
Wanachama wa chama kipya cha ACT-Tanzania waliosafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Mtwara wakitumia basi dogo aina ya Coaster walikumbana na kipigo kutoka kwa wafuasi wa CUF waliowazuia wakidai kuwa hawakualikwa.
Mmoja wa wanachama wa ACT ambaye pia ni Mwenyeji wa Mkoa Kigoma anayeishi Dar es Salaam, Monalisa Ndala alisema; “Tuliambiwa huu mkutano siyo wa kwetu na ACT hawahusiki, ndipo walianza kutupiga wakitutaka kuvua sare kama tunataka kuendelea na msafara.”
Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa