Home » » MKANDARASI LAWAMANI KUJENGA BARABARA CHINI YA KIWANGO MTWARA

MKANDARASI LAWAMANI KUJENGA BARABARA CHINI YA KIWANGO MTWARA

Baadhi ya wananchi mkoani Mtwara wameulalamikia uongozi wa manispaa na wilaya kushindwa kusimamia ujenzi wa barabara kiasi cha kujengwa chini ya kiwango licha yakutakiwa kujengwa katika viwango vya kimataifa.
Hali hiyo imekuja baada ya mkandarasi wa Kampuni ya DB Shaprya anayejenga barabara ya Kunambi inayotoka soko kuu hadi bandarini kuwa chini ya kiwango, hivyo kuanza kuharibika mapema sambamba na mifereji kutokupitisha maji.
Ahmad Said mkazi wa Railway, alisema kuwa barabara hiyo imejengwa kwa viwango hafifu hivyo kushindwa kuelewa viongozi wanaohusika na utoaji wa tenda za kazi kwani wamekuwa wakitoa zabuni kwa wakandarasi wenye kazi nyingi hivyo kushindwa kufanya kazi kwa kiwango kinachotakiwa.
“Tunashindwa kuelewa viongozi wanaohusika na utoaji wa tenda tulishangaa sana kuona kokoto zikimwagwa na makarai badala ya magari kutokana na ukosefu wa vitendea kazi na haya ndiyo matokeo yake barabara zinakuwa chini ya kiwango na zinazotumika ni pesa zetu,” alisema Said.
Akizungumzia hali hiyo, Mwenyekiti wa Serikali za Mtaa wa Serengeti, Zuhura Majdi alisema kuwa hali hiyo waliiona lakini hakuwa na uwezo wa kuizungumzia na kwamba baada ya kuapishwa tatizo hilo atalifikisha kwenye kata kuona ni kwa namna gani barabara inatengenezwa kwa kiwango kinachostahili.
“Hili tatizo tuliliona na baada ya mvua kunyesha ndiyo barabara inazidi kufumuka hivyo kwa kuwa tayari nimeapishwa nitalibeba kwenda kata ili lifuatiliwe kuona nini kinafanyika kwa sababu kama hivi mvua zimeanza kunyesha tayari sehemu zilizo karibu na mifereji tayari zimefumuka,” alisema Majdi. Kwa upande wake, Meya wa Manispaa hiyo, Suleiman Mtalika alipotafutwa juu ya hilo alitaka atafutwe mkuu wa wilaya.
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa