Home » » WAFANYABIASHARA MASASI KUANZA KULIPA KODI BENKI

WAFANYABIASHARA MASASI KUANZA KULIPA KODI BENKI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Masasi mkoani Mtwara limeitaka halmashauri hiyo kuweka utaratibu kwa wafanyabiashara wilayani humo kulipa kodi zao kwa njia za miamala ya kibenki ili kudhibiti mianya ya rushwa na kuweza kukusanya mapato yake ya ndani kwa wingi zaidi.

Madiwani hao walitoa mapendekezo hayo jana wakati walipokuwa wakichangia muhtasari wa kamati ya kudumu ya uchumi kwenye kikao cha kawaida cha baraza la madiwani lililofanyika katika ukumbi wa halmashauri hiyo mijini hapa.

Walisema kuwa ili kuweza kudhibiti mianya ya rushwa na kukusanya mapato mengi zaidi katika halmashauri hiyo yanayotokana na kodi mbalimbali zinazolipwa na

wafanyabiashara ni wakati mwafaka sasa kwa uongozi kuweka utaratibu wa kumtaka kila mfanyabiashara kulipa kodi kwa kutumia njia za kibenki badala ya kulipa kwa njia ya malipo keshi.

Walisema kwa utaratibu wa sasa kwa wafanyabiashara kulipa kodi zao kwa kutumia malipo keshi kupitia kwenye madirisha ya ofisi za fedha za halmashauri ni kuendelea kuweka mianya ya rushwa na kuikosesha mapato halisi yanayotakiwa kuyapata katika makusanyo yake ya ndani.

Kwa upande wake diwani wa Kata ya Chanikanguo Samson Bushiri alisema iwapo wafanyabiashara wilayani humo wakianza kulipa kodi benki mapato ya halmashauri yatakusanywa kwa wepesi zaidi na kuondoa hali ya wasiwasi kwa madiwani kuhusu ukusanyaji wa mapato ya ndani.

Alisema wao kama madiwani wameingiwa na wasiwasi kuhusu utaratibu huo kwa wafanyabiashara kulipa kodi zao kwenye ofisi za halmashauri kwani mara kadhaa wameshuhudia kuwepo kwavitabu tofauti tofauti vinavyotumika kulipa kodi kwa wafanyabiashara jambo ambalo linawapa wasiwasi madiwani hao juu ya ukusanyaji wa mapato yake ya ndani.

“Kuanzia sasa halmashauri iweke utaratibu wa kila mfanyabiashara kwenda kulipa kodi zake benki kuliko kuendelea kulipa ndani ya ofisi hii itasaidia kupunguza mianya ya rushwa na hata kuiwezesha kupata mapato yake ya ndani kwa wingi zaidi,”alisema Bushiri.

Naye diwani wa Kata ya Nanjota, Eduward Mmavele alisema utaratibu huo utasaidia kuifanya halmashauri kupata mapato yake kwa wingi zaidi na kwamba utaratibu huo ni wa usalama zaidi na ndio wa kisasa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Beatrice Dominic alipongeza mapendekezo hayo na kudai kuwa iwapo utaratibu huo ukiridhiwa na madiwani utaanza kutekelezwa mara moja na kwamba kuanzia sasa wataanza kuwahamasisha wafanyabiashara kwenda kulipa benki kodi zao.

“Kwa upande wangu hata mimi naumia sana kichwa juu ya utaratibu wa wafanyabiashara kulipa kodi zao hapa ofisini hivyo ninyi madiwani kama mmeliona hili basi itakuwa vizuri kubadilisha utaratibu huu na sasa kila mfanyabiashara tutamueleza akalipe benki,”alisema Dominic.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa