Home » » Mtendaji wa kijiji auawa kwa mapanga

Mtendaji wa kijiji auawa kwa mapanga

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Zelothe Steven.
Kundi la watu wasiofahamika, wamemuua kwa kumcharanga mapanga, Mtendaji wa kijiji cha Chakama kata ya Mwenge, Halmashauri ya mji wa Masasi mkoani Mtwara, Selemani Eckoni (32).
Mtendaji wa kijiji cha Mwenge, Mely Karim, alisema kuwa tukio hilo la kinyama lilitokea usiku wa kuamkia jana katika kijiji cha Mwenge wakati mtendaji huyo akiwa nyumbani kwake amejipumzisha.

Karim alisema taarifa za kuuawa kwa mtendaji huyo zilianza kuenea kijijini hapo jana asubuhi baada ya baadhi ya watu kusikia sauti ya mtoto wa marehemu, Makala Selemani (6), mwanafunzi wa Shule ya Msingi Mwenge akipiga mayowe kuomba msaada baada ya yeye kuona baba yake akiwa amelala nje ya nyumba yao akivuja damu kichwani huku pembeni yake kukiwa na kitanda cha kamba.

Alisema kufuatia mayowe ya mtoto huyo, wananchi walikusanyika katika nyumba ya marehemu na kukuta mtendaji huyo tayari amefariki dunia huku akiwa na majeraha makubwa kichwani.

Alisema baada ya watu hao kufanya mauaji hayo, waliingia ndani ya nyumba ya marehemu na kuchukua pikipiki moja aina ya Sanlg, deki moja ya televisheni na simu aina ya Nokia.

Kaka wa marehemu, Hassan Issa, alisema alipelekewa taarifa za kuuawa kwa ndugu yake akiwa nyumbani kwake.

Issa alisema alikwenda nyumbani kwa marehemu na kupiga simu polisi kuelezea taarifa za mauaji hayo.

Kamanda wa Polisi mkoani Mtwara, Zelothe Steven, alithibisha kutokea kwa mauaji hayo.

Hata hivyo, Kamanda Steven alisema chanzo cha mauaji hayo hakijafahamika na hakuna mtu yeyote anayeshikiliwa kuhusiana na mauaji hayo.

Baadhi ya ndugu wa marehemu wameliambia NIPASHE kuwa wakati wa uhai wake, mtendaji huyo aliyeacha watoto wanne, alikuwa akiishi peke yake.
 
SOURCE: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mtwara yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa